Kampuni yatoa zawadi kumtafuta aliyeiba lori zima la bia

Chanzo cha picha, Getty Images
Kampuni ya kutengeneza bia ya Pabst Brewing Company imegeukia mitandao ya kijamii kuomba msaada wa kutafuta maelfu ya makopo ya bia yake ya Pabst Blue Ribbon (PBR) yaliyoibwa kutoka kituo cha usambazaji huko California.
"TUMEIBIWA," kampuni hiyo ilitangaza. "Kwa mwizi huyo: hatukulaumu kwa kutaka kujivunia kwa marafiki zako kuhusu kiasi kikubwa cha bia ya PBR ulicho nacho, tunatamani tu ungeipata kwa njia halali na ya heshima."
Kwa mujibu wa polisi, mtuhumiwa aliwasilisha nyaraka bandia katika kituo cha usambazaji cha Anheuser-Busch mjini Montclair na kufanikiwa kuondoka na mzigo wa bia wenye thamani ya dola za Marekani 25,000 (takriban pauni 18,500), ambao ulikuwa umepangwa kupelekwa San Diego.
Pabst imesema "inafuatilia kwa karibu sana" tukio hilo ambalo imeeleza kuwa ni "la kushangaza na la kipuuzi", na sasa inatoa zawadi kwa yeyote atakayesaidia kupatikana kwa bia hiyo yenye uzito wa pauni 40,000 (sawa na kilo 18,144).
Polisi wa Montclair walisema kuwa huo ulikuwa wizi wa pili kutokea siku hiyo hiyo katika kituo hicho hicho cha usambazaji. Wapelelezi wanachunguza iwapo matukio hayo mawili yalikuwa sehemu ya operesheni moja ya uporaji wa mizigo kwa kutumia nyaraka za udanganyifu.
Katika tukio la kwanza, mzigo wenye thamani ya dola 45,000 (takriban pauni 33,000) uliokuwa ukielekea Tucson, Arizona, ulichukuliwa tarehe 17 Agosti lakini haukuwahi kufika ulipokusudiwa hata baada ya wiki mbili.
Saa moja baadaye, polisi wanasema kuwa wezi walitumia nyaraka bandia kuchukua mzigo wa bia ya Pabst Blue Ribbon.
"Wachunguzi wamebaini kufanana kwa matukio haya mawili," polisi walisema. "Taarifa zilizotolewa kuhusu kampuni ya usafirishaji, dereva na magari yaliyohusika zina dosari na tofauti zinazoshukiwa, na kwa sasa zinaendelea kuchunguzwa."



